Tuesday 18 March 2014

Airtel yakabidhi Sh Mil 5 Tuzo za Mwanamakuka 2014

Afisa Uhusiano wa Airtel, Jane Matinde (kushoto) akimkabidhi mfano wa hundi Mwenyekiti UWF na Mratibu wa Mradi wa Tuzo za Mwanamakuka Maryam Shamo wakati wa hafla ya Tuzo za Mwanamakuka 2014 ambapo Airtel Tanzania ni moja kati ya Wadhamini wa tuzo hizo ambazo Leila Mwambungu  aliibuka mshindi wa mwaka 2014. Wengine pichani kulia ni Mkurugenzi  Mkuu wa TWB Bi Margreth Chacha.
Afisa Uhusiano wa Airtel, Jane Matinde (kulia) akimpongeza mshindi wa tuzo ya Mwanamakuka 2014 Leila Mwambungu mara baada ya kutangazwa katika hafla iliyofanyika Escape One, Mikocheni Dar es Saalam.
Mshindi wa Tuzo za Mwanamakuka 2014, Leila Mwambungu akitoa shukrani zake mara baada ya kutangazwa katika hafla iliyofanyika Escape One siku ya Jumamosi. Kulia kwake ni Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Wanawake Tanzania (TWB) Margreth Chacha.
KAMPUNI ya simu za mkononi ya Airtel, imekabidhi waandaaji wa Tuzo za Mwanamakuka, Umoja wa Wanawake Marafiki (UWF) kiasi cha Sh. Mil. 5 wakati wa hafla ya utoaji wa tuzo za Mwanamakuka-2014 zilizofanyika jijini Dar es Saalam, ambapo Leila Mwambungu aliibuka mshindi wa mwaka huu akiwabwaga washiriki wenzake tisa aliochuana nao.
Tuzo ya mwaka huu ilishirikisha washindi 10, watano wa mwaka 2012 na wengine wa mwaka 2013 kupima mafanikio yao kibiashara baada ya kunyakua tuzo na zawadi ya fedha katika shindano hilo lililoasisiwa mwaka juzi.
Mshindi huyo aliyekuwa mshindi wa pili wa tuzo za mwaka jana, aliibuka kidedea baada ya barua iliyoeleza alipotokea, alipo na malengo yake baada ya kushinda tuzo hiyo kutia fora na kumpa ushindi mbele ya wenzake.
Kampuni ya Airtel, imekuwa ikidhamini tuzo hizo tangu zilipoanzishwa safari hii ilikabidhi kiasi hicho cha fedha kupitia kwa Afisa Uhusiano wake, Jane Matinde aliyeeleza furaha waliyonayo kudhamini tuzo hizo kwa miaka mitatu mfululizo.
Matinde alisema Airtel wanajisikia faraja kuona wamekuwa sehemu ya kuleta mabadiliko kwa wanawake kupitia tuzo hiyo na kuahidi kuendelea kushirikliana na UWF kuhakikisha mabadiliko hayo yanawafikia wanawake wengi zaidi nchini.
“Tutaendelea kushirikiana na UWF, ili kuhakikisha tunawafikia wanawake wengi zaidi nchini,” alisema Matinde.
Kwa upande wa mshindi wa Mwanamakuka 2014, Leila Mwambungu alisema amejisikia furaha sana kushinda tuzo hiyo akidai hakuwa ametegemea na kuwashukuru waandaaji na wadhamini wake na kuomba waendelee kuwasaidia kuwakwamua wanawake nchini ambao wamejitosa kwenye shughuli za ujasiriamali.
"Naona fahari na furaha kuwa mshindi wa tuzo hizi za mwanamakuka kwa mwaka huu, napenda kuwashukuru sana waandaaji wa tuzo hizi kwa kuniona kupitia juhudi ninazoziweka katika kazi zangu na biashara zangu. Mpaka sasa nimeweza kuajiri watanzania kupitia biashara zangu. Kiasi nilichozawadiwa kitanisaidia kukuza zaidi mtaji wangu. Nashukuru sana," alisema mshindi huyo.
Naye Mwenyekiti UWF na Mratibu wa Mradi wa Tuzo ya Mwanamakuka, Mariam Shamo alisema tuzo hiyo inaendelea kukua na kuzidi kuiboresha na kudai lengo la shindano la mwaka huu lilikuwa kupima maendeleo ya washindi wao 10 kuona jinsi gani biashara zao zinavyosonga mbele baada ya kumzawadia aliyefanya vizuri zaidi.
"Tunashukuru sana Airtel kwa kushirikiana nasi miaka mitatu kwa sasa na tunaamini kuwa bado wataendelea kutoa mchango wao na kushirikiana nasi na kutuunga mkono kwa miaka mengine ijayo na kuhakikisha lengo letu la kumwinua mwanamke wa kitanzania linafikiwa," alisema Mariam.
Washiriki wa tuzo za mwaka huu walikuwa ni Tatu Ngao, Mwananne Msekalile, Sikudhani Daudi na Nasra Aziz walioshinda mwaka 2012 na Aziza Mbogolume, Leila Mwambungu, Theonistina Renatus, Maajab Yusufu na Agnes Daudi walioshinda mwaka 2013.

Monday 17 March 2014

Wanawake msiwe tegemezi kwa kigezo cha kukosa ajira



Wanawake hawapaswi kuwa wanyonge
 WANAWAKE wametakiwa kutokuwa tegemezi kwa kigezo cha kukosa ajira, badala yake wajiunge katika vikundi  vya ujasiriamali ili kujenga misingi  bora ya familia zao.
Akizungumza jijini Dar es Salaam  juzi, Mratibu wa shirika lisilo la kiserikali Caritas linajihusisha na utoaji wa miradi  mbalimbali kwa kina mama, Glads Oning’o, alisema mwanamke ni nguzo ya familia, hivyo wajishughulishe ili kuzisaidia familia zao.
Alisema shirika hilo lina miradi ya kuwakopesha fedha kina mama  pamoja na mradi wa kilimo, ili waweze kujikomboa, kuondokana na hali tegemezi.

Huyu ndiye Mwanamakuka 2014

Hii ilikuwa mwaka jana niliponyakua ushindi wa pili
Wakati nakabidhiwa hundi ya ushindi wangu wa mwaka jana
Nikiwa na washindi wenzangu wa mwaka jana, Theonistina Renatus na Aziza Mbogolume
SIKU ya Jumamosi pale Escape One, kulifanyika Family Day iliyoambatana na utoaji wa Tuzo za Mwanamakuka 2014 inayoratibiwa na Umoja wa Wanawake Marafiki (UWF) chini ya udhamini wa Benki ya Wanawake Tanzania (TWB) na Airtel na wengineo.
Kwa tuzo zilifana mno, lakini kubwa ni kwamba mshindi wa Tuzo ya Mwanamakuka kwa 2014 hatimaye alipatikana baada ya washiriki 10 walioshiriki na kushinda tuzo za mwaka 2012 na 2013 kushindanishwa kuandika barua kuonyesha kufanikiwa kwake na kufikia malengo baada ya ushindi waliopata miaka hiyo.
Miongoni mwa washiriki nilikuwa mimi mwenyewe Leila Mwambungu, mshindi namba mbili wa mwaka jana ( 2013).
Bahati nzuri, Mungu alikuwa upande wangu baada ya kuibuka kidedea dhidi ya washiriki wenzangu.
Kwa hakika namshukuru Mungu kwa kuweza kunisaidia kushinda tuzo ya Mwanamakuka kwa mwaka 2014 na kama nilivyoandika katika barua yangu nitajitahidi kwa uwezo wa Allah (Subhanna Wataallah) kuwa mfano katika tuzo hizo na kuwasaidia wanawake wengine kuhamasisha kujikomboa kupitia ujasiriamali.
Tuzo hii ya Mwanamakuka ilianzishwa mwaka 2012 na Tatu Mwenda ndiye aliyeibuka kidedea mwaka huo wa kwanza akifuatiwa na Mwanne Msakalile.Mwaka jana mshindi wa kwanza alikuwa Aziza Mbogolume na kufuatiwa na mimi mwenyewe na nishukuru kwamba ushindi wa mwaka jana umeniwezesha kufikia malengo niliyokusudia, japo bado naendelea kupigana.
Ushindi wa mwaka huu ambao kwa hakika sikuutegemea kutokana na ushindani uliokuwapo kwa kujumuishwa washindi wote 10, watano wa mwaka 2012 na wengine wa mwaka jana.
Niwashukuru waratibu wa tuzo hiyo Umoja wa Wanawake Marafiki (UWF) na wadhamini wakuu Benki ya Wanawake Tanzania (TWB).
Pia shukrani zangu ziende kwa wote waliosaidia kwa namna moja wa nyingine kupata ushindi kwa miaka miwili mfululizo, hususani Mume Wangu ambaye amekuwa akinitia Moyo na kuwa bega kwa bega katika michakato hii na hata ninapovunjika moyo hunitia nguvu na kunisisitiza kuwa 'Wanawake Wanaweza na Katu Hawakati Tamaa'.
Kwa washiriki wenzangu wanashukuru pia na kuwataka tuendelee kushirikiana kuonyesha mfano kwa wengine na kujaribu kuwasaidia wanawake wengine nao wafikie malengo kama tulivyowezeshwa na UWF na TWB na hasa Bi. Mariam Shamo na Margareth Chacha.

Tusiruhusu ushoga nchini, hatari kwa taifa-Sheikh Muhenga



http://bloggerimports.files.wordpress.com/2008/12/img_2954-raisidd.jpg?w=640
Sheikh Mohammed Muhenga
SERIKALI imeombwa kufuata nyayo za serikali ya Uganda chini ya Rais Yoweri Museveni kwa kuktaa kuruhusu ushoga.
Serikali imeombwa kufuata nyayo za serikali ya Uganda chini ya Rais Yoweri Museveni kwa kukataa kuruhusu ushoga licha ya kuziudhi nchi za magharibi zinazokingia kifua vitendo hivyo.
Ombi hilo limetolewa na Imamu wa Msikiti wa Mwembechai, Sheikh Mohammed Muhenga, alipokuwa akiwahutubia waumini kabla ya swala ya Ijumaa iliyoswaliwa msikiti hapo, jijini Dar es Salaam.
Imamu Muhenga alisema kitendo cha Watanzania kunyamazia na kukumbatia matendo maovu yanayomchukiza Mungu vinaweza kuzua balaa kwa taifa.
"Tushirikiane kukemea maovu, tusinyamazie matendo yanayomchukiza Mungu kwani hakuna anayeweza kuhimili ghadhabu za Mungu akiamua kutuadhibu,"alisema .
Sheikh huyo alisema vitendo vya ulevi, biashara ya watu kujiuza, ujambazi na matendo mengine kwa kisingizio cha kukabiliana na hali ngumu ya maisha vinapaswa kuepukwa kwa nguvu zote.
"Huku ni sawa na kumbeep Mungu, je akiamua kutupigia tupo tayari kuhimili ghadhabu yake, tukemee maovu na kukemea kwani Mtume Muhammad (Sallallah Aley Wasalam) anasema miongoni mwa dalili 10 za kiama ni umma wake kugeuza pombe kuwa chai, watu kurejea enzi za Kaum Lut," alisema.
Sheikh alisema matendo vya ushoga na maovu mengine ni kuvuka mipaka kwa wanadamu ya uumbaji na humchukiza Mungu, hivyo ni wajibu wa kila mtu kukemea na kuyakataa matendo hayo.
Hivi karibuni Uganda ilipitisha sheria kali dhidi ya vitendo vya ushoga na kukera nchi ya Marekani na washirika kwake ambao wameruhusu vitendo hivyo katika nchi zao licha ya kwenda kinyume na mafundisho ya kidini.
Katika vitabu vya kuanzia Qur'an mpaka Biblia inasimulia kisa cha watu wa Nabii Lutu walivyotakabari na kuwaendea wanaume wenzao wakiwaacha wanawake na Mungu akawaadhibu adhabu inayoelezwa haijawahi kupewa wanadamu kama hiyo.

Saturday 22 February 2014

HII NDIYO TOP 10 YA WALIONG'ARA KIDATO CHA NNE

http://1.bp.blogspot.com/-SUcYdsp6pq0/UU7zJboieNI/AAAAAAAAdo4/5fAU57VdG3M/s1600/NECTA.jpg
WASICHANA Wasichana waliofanya vizur kwenye mtihani huo wameongozwa na Robina Nicholaus (Marian Girls), Magrath Kakoko (St Francis), Joyceline Leonard Marealle (Canossa), Safarina W Mariki, Abby T Sembuche na Janeth Urassa (Marian Girls). Wengine ni Angle Ngulumbi (St Francis), Getrude James Mande wa Precious Blood (Arusha), Violet Mwasenga wa St Francis na Catherine Swai kutoka Marian Girls.
WAVULANA
Wavulana waliofanya Vizuri ni Sunday Mrutu wa Anne Marie, Nelson Rugola Anthony na Emanuel Mihuba Gregory wote kutoka Kaizirege, Razack Hassan wa St Matthew’s (Pwani) na Hamis Msangi kutoka Eangles (Pwani).
Wengine ni Joshua Zumba wa Uwata (Mbeya), Brian Laurent na Mohamed Ally wa Marian Boys (Pwani), Shahzill Msuya wa St Amedeus (Kilimanjaro) na Shabani Hamisi Maatu wa Mivumon Islamic Seminary (Dar es Salaam).

UWF yahamasisha wanawake kushiriki Siku ya Wanawake Duniani, Family Day


  MENEJA wa Tuzo ya Mwanamakuka ambaye pia ni Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Marafiki (UWF) Mariam Shamo akifafanua jambo mbele ya washindi wa tuzo hiyo wa mwaka juzi na jana pamoja na wanahabari kuhusiana na hafla yao wanayoitarajia kuifanya siku ya Familia 'Family Day' Machi 15 mwaka huu,ambayo imepangwa kufanyika ndani ya kiota kipya cha maraha na burudani Escape One Mikocheni jijini Dar, pembeni yake ni  Mdau mkubwa wa tuzo hizo na Mkurugenzi wa Benki ya Wanawake Tanzania Margareth Chacha.

Mjumbe wa Mradi wa Mwanamakuka (Mwanamakuka Awards) na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Wanawake Tanzania,Bi. Margareth Chacha akisisitiza jambo mbele ya washindi wa Mwanamakuka mwaka 2012 na 2013 alipokuwa akiongelea siku ya Familia  Duniani tarehe 15 mwezi ujao mbele ya waandishi wa habari jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki. Kushoto ni Meneja wa Mradi wa Mwanamakuka ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kituo cha Wanawake Marafiki (Unit of Women Friends),Bi Maryam Shamo.
WASHINDI wa Tuzo ya Mwanamakuka mwaka 2012 na 2013 wakiwa pamoja wakati walipokutana na waratibu wa shindano hilo kwa ajili ya kujipanga na Siku ya Wanawake Duniani inayotarajiwa kufanyika mnamo Machi 8 na kufuatiwa na Family Day Machi 15 mwaka huu.
WANAWAKE nchini wamehamasishwa kushiriki Siku ya Wanawake Duniani itakayofanyika Machi 8, na kufuatiwa na Family Day Machi 15, mwaka huu jijini Dar es Salaam na kujadili masuala mbalimbali ya kumwezesha mwanamke.
Mjumbe wa mradi wa Mwanamakuka (Mwanamakuka Award) na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Wanawake Tanzania, Margareth Chacha, aliwaambia waandishi wa habari mwishoni mwa wiki kuwa siku hiyo ni ya muhimu kwa wanawake kwa vile itawaleta pamoja na kujadili masuala mbalimbali.
“Tutakutana Siku ya Wanawake Duniani na kujadili namna bora zaidi ya kumuwezesha mwanamke kujiinua kiuchumi,” alisema.
Alisema benki yake inafadhili washindi wanawake wajasiriamali kupitia mradi huo na inafanya hivyo kwa ajili ya kumwinua mwanawake kupitia benki yao ya wanawake.
Alisema benki hiyo inataka kuona wanawake wengi wanaingia katika shughuli za kijasiriamali na pia imejipanga kutumia matawi yake nchini kupanua wigo wa zawadi ya Mwanamakuka.
Alisema mpaka sasa ni asilimia mbili tu ya wanawake wanaotumia huduma za kibenki kati ya asilimia nane ya Watanzania wote wanaotumia huduma hizo, na sasa wakati umefika kuongeza idadi ya wanawake.
“Hali hiyo ni ya kihistoria lakini kwa sasa wanawake tunashukuru hali imebadilika tunaweza kufanyakazi mbalimbali zikiwamo za biashara,”aliongeza.
Alisisitiza umuhimu wa wanawake kujiunga katika vikundi kwa ajili ya kupata mikopo kutoka katika benki yao kufanyia shughuli zao za kijasiriamali.
Naye Meneja wa mradi wa Mwanamakuka ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kituo cha Wanawake Marafiki (UWF),  Maryam Shamo, alisema Siku ya Wanawake Duniani kutakuwa na maonyesho ya kazi za kijasiriamali za wanawake na michezo mbalimbali.
“Siku hiyo washindi wa mwaka huu watapatiwa zawadi zao, na pia mshindi wa jumla wa mwaka 2012 na 2013 atapatiwa zawadi kati ya washindi kumi waliokwisha pata zawadi,'' alisema.
Alifafanua kuwa katika kusherehekea ya siku hiyo, watu wengi wamealikwa wakiwamo akinamama wajasiriamali na wanasiasa wanawake.
Kwa upande wake, mjasiriamali mkazi wa Dar es Salaam na mshindi wa nyuma wa mradi huo, Tatu Ngao, alisema alishinda Shilingi  milioni sita ambazo zimemwezesha kufanya biashara yake kwa ufanisi.
“Nilishinda kupitia biashara yangu ya kutengeneza keki...nimepanuka kwa kiwango cha kuridhisha hadi sasa,” alisema.
Zawadi ya Mwanamakuka ni mradi uliobuniwa na Kituo cha Wanawake Marafiki kwa ajili ya kuwawezesha wajasiriamali wanawake kwa ufadhili wa Benki ya Wanawake Tanzania na wadau wengine.

Hata ndiyo matokeo ya kidato cha nne kwa mwaka 2013

 
Kaimu Katibu Mkuu wa baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA), Dk. Charles Msonde akisoma matokeo ya mitihani ya kidato cha nne mwaka 2013 Dar es Salaam jana. 


Idadi ya ufaulu mtihani kidato cha nne mwaka jana  imeongezeka kutoka 185,940  hadi kufikia 235, 225, ikilinganishwa na mwaka 2012.
Vile vile watahiniwa 151,187 kati ya 404,083 waliofanya mtihani wa kidato cha nne mwaka jana wamepata ‘divisheni’ ziro.

Hata hivyo,  idadi ya waliopata daraja sifuri imepungua ikilinganishwa na mwaka 2012 ambapo wanafunzi 240,903 kati ya 397,132 waliambulia daraja hilo na kusababisha hamaki iliyoshinikiza viongozi wa sekta ya elimu kuwajibishwa.

Matokeo hayo yalitangazwa jana jijini Dar- es- Salaam na Kaimu Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la  Mitihani (Necta), Dk. Charles Msonde, aliyeongeza kuwa idadi ya ufaulu kwa mwaka jana ilipanda ikilinganishwa na mwaka 2012.

Ongezeko hilo la watahiniwa 49,285 waliofaulu zaidi mwaka huo, limefanya kiwango cha ufaulu kupanda kwa asilimia 58.25 ikilinganishwa na hali ilivyokuwa  mwaka 2012.

“Jumla ya watahiniwa  404,083 sawa na asilimia 94. 48 waliofanya mtihani huo, wanafunzi 151,187 ambao ni  asilimia 42.91 walishindwa mtihani.” Alisema Dk. Msonde na kuongeza kuwa wasichana waliofaulu ni 106,792 sawa na asilimia 56.73,  wavulana ni 128,435 sawa na asilimia 59.58.

Watahiniwa  waliofaulu  moja kwa moja kutoka shuleni ni 201,152 sawa na asilimia 57.09, wasichana wakiwa 90,064 sawa na asilimia 55.49 na wavulana ni 111,088 sawa na asilimia 58.45.

Alisema idadi ya wanafunzi  wa kujitegemea ilikuwa   34,075 sawa na asilimia 66.23 ikilinganishwa na  ya mwaka 2012 ambao idadi yao ilikuwa 2,619.

Watahiniwa wa mtihani wa Maarifa(QT), waliofaulu ni 6,529 sawa na asilimia ikilinganisha na watahiniwa 5,984  wa  mwaka 2012.

Akitangaza matokeo hayo mbele ya wanahabari alisema watahiniwa  walioandikishwa kufanya mtihani huo mwaka jana walikuwa 427,679, kati yao wasichana ni  199,123 sawa na asilimia 46.56.

Wavulana walikuwa ni 228,556 sawa na asilimia 53.44, huku watahiniwa wa shule wakiwa 367,163 na watahiniwa wa kujitegemea wakiwa 60,516.

Alisema kati ya watahiniwa 427,679 waliosajiliwa kufanya mtihani huo, 404,083 sawa na asilimia 94.48 walifanya mtihani huo na watahiniwa 23,596 sawa na asilimia 5.52 hawakufanya mtihani huo.

Kwa watahiniwa wa shule 367,163 waliosajiliwa , 352,614 sawa na asilimia 96.04 walifanya mtihani, wasichana wakiwa 162,412 sawa na asilimia 96.07 na wavulana ni 190,202 sawa na asilimia 96.0.

Pia alisema watahiniwa 14,549 sawa na asilimia 3.96 hawakufanya mtihani.

Aidha aliongeza kuwa kwa upande wa watahiniwa wa kujitegemea 60,516 waliosajiliwa  kufanya mtihani huo, 51,469 sawa na asilimia 85.05 walifanya mtihani huo, na watahiniwa  9,047 sawa na asilimia 14.95 hawakufanya mtihani.

Alisema  kwa  watahiniwa  18,217 wa mtihani wa maarifa (QT),  waliosajiliwa, 15,061 sawa na asilimia 82.68 walifanya mtihani huo na 3,156 sawa na asilimia 17.32 hawakufanya mtihani.

Kwa upande wa ubora wa ufaulu kwa kuangalia madaraja , alisema kwa watahiniwa wa shule unaonyesha kuwa jumla ya watahiniwa 74,324 sawa na asilimia 21.09 wamefaulu katika daraja la I hadi la III wakiwamo wasichana 27,223 sawa na asilimia 16.77 na wavulana 47.101 sawa na asilimia 24.

Dk. Msonde alisema takwimu za matokeo zinaonyesha kuwa ufaulu katika masomo yote umepanda kwa asilimia kati ya 0.61 na 16.72 ikilinganishwa na mwaka 2012.

Alisema watahiniwa wamefaulu zaidi masomo ya Kiswahili kwa asilimia 67.77 na somo ambalo wamefaulu kwa kiwango cha chini ni Hesabu kwa asilimia 17.78.

Kwa mujibu wa Necta wanafunzi waliong’ara ni Robina Nicholaus, Sarafina Mariki, Abby Sembuche   na  Janeth Urassa  wa Sekondari ya Wasichana ya Marian.

Wengine ni  Magreth Kakoko na Angel Ngulumbi wa   St. Francis, Joyceline Marealle wa Sekondari ya  Canossa,   Sunday Mrutu  wa Sekondari ya Anne Marie,  Nelson Rugola na Emmanuel Mihuba Sekondari ya  Kaizirege .

Kadhalika, shule zilizofanya vizuri zaidi  na kuingia katika kumi bora  katika kundi la shule zenye watahiniwa 40 ni  shule ya wasichana ya St. Francis, Shule ya wavulana na Marian, shule ya wasichana ya Feza, shule ya Precious Blood, Canossa, Shule ya wasichana ya Marian, shule ya wasichana ya Anwarite, Abbey, Rosminini na Shule ya Seminari ya Don Bosco.

KUANGALIA MATOKEO YA MITIHANI



Matokeo ya Mtihani wa Kidato cha Nne (CSEE) uliofanyika Novemba 2013 unaweza kuyaona kwa  kubofya hapa MATOKEO