Wednesday 3 April 2013

DC ASHAURI 'NIACHE NISOME' IWE TAASISI KUWALINDA WASICHANA KIELIMU



Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Muhingo Rweyemamu.
MKUU wa Wilaya ya Handeni, Muhingo Rweyemamu ameshauri kampeni aliyoianzisha wilayani humo yenye kauli ya 'Niache Nisome' kupambana na mimba kwa wanafunzi ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa jamii juu ya umuhimu wa elimu, iwe taasisi na kufanya shughuli zake nchi zima.

Rweyemamu aliyasema hayo hivi karibuni alipokuwa akifanya mahojiano na mwandishi wa habari hizi juu ya hali ilivyo kwa sasa ya matukio ya mimba kwa wanafunzi na kukatishwa masomo, vitendo ambavyo alivikuta vikishamiri eneo hilo hasa mwanzoni mwa mwaka jana kabla ya uteuzi wa nafasi hiyo.

Akizungumzia kampeni ya 'Niache Nisome' aliyoianzisha muda mfupi baada ya kuteuliwa na Rais Jakaya Kikwete kuiongoza wilaya hiyo, alisema kampeni yake imekuwa na mafanikio kwani licha ya matukio ya mimba kupungua wananchi wameipokea vizuri kampeni hiyo.

Alisema wananchi hasa baadhi ya wazazi wamekuwa wakiripoti matukio ya mimba na kutoa ushirikiano pale inapoitajika ili wavunjaji sheria kwa wanafunzi waweze kuadhibiwa kitendo ambacho hapo awali kilikuwa kigumu, na hata wengine kushirikia mikakati ya kuwaachisha masomo wanafunzi.

"Nina furahi kuwa muitikio wa kampeni ya 'Niache Nisome' katika maeneo mengi ya wilaya yangu imepokelewa vizuri, wananchi wanaanza kutambua umuhimu wa elimu na wanatoa ushirikiano kwa wale wachache wanaokwenda kinyume kwa kuwakatisha masomo wanafunzi hasa wa kike...jamii ya hapa wengi wao mwanzoni ilikuwa ni kitu cha kawaida mwanafunzi kulala nje pasipo idhini ya wazazi wake," alisema Rweyemamu akizungumza.

Akizungumzia utekelezaji wa kampeni hiyo Mkuu wa wilaya alisema licha ya kamatakamata iliyokuwa ikifanyika kwa wazazi, wanafunzi na watu waliyokuwa wakisababisha mimba kwa wanafunzi viongozi na watendaji anuai wa halmashauri hiyo walizunguka maeneo mengi na kutoa elimu juu ya umuhimu wa elimu kwa jamii zima.

"Tulikamatana sana mwaka jana kuanzia mwezi wa nane na kwa muda mfupi tulikuwa tuna watuhumiwa 80 wakiwemo wazazi, watu waliokuwa wakidaiwa kusababisha mimba kwa wanafunzi pamoja na wanafunzi wenyewe...mimi mwenyewe nilitembelea baadhi ya shule nikitoa elimu lakini baadaye walielewa licha ya uwepo wa changamoto kadhaa," alisema kiongozi huyo wa Wilaya ya Handeni.

Aidha akifafanua zaidi alisema ipo haja ya kampeni hiyo kugeuzwa taasisi na kuanza kufanya shughuli zake nchi nzima ili kampeni kama hiyo iweze kuyanufaisha maeneo mengi ambayo yamekuwa na mwamko duni wa elimu kwa jamii. Aliongeza kuwa faida ya kampeni hiyo haipiganii elimu kwa mtoto wa kike pekee kwani inagusa maeneo mengine pia kama miundombinu ya shule, vitendea kazi na vifaa vingine muhimu kwa shule kiujumla. 

Hata hivyo kiongozi huyo alisema licha ya kuanza kufanikiwa katika kampeni hiyo bado suala la ufauli katika shule za sekondari hasa kidato cha nne ni tatizo kutokana na ilivyokuwa hapo awali. Alisema matokeo ya mtihani wa kidato cha nne mwaka jana (2012) yalikuwa mabaya sana kwani Wilaya nzima ya handeni haikuwa na daraja la kwanza. 

"changamoto iliyobaki sasa ni ufaulu...matokeo ya kidato cha nne kwa mwaka jana wilaya nzima ilikuwa na ziro 246, hatukuwa na daraja la kwanza kabisa huku tukipata wanafunzi 2 tu walio na daraja la pili," alisema Rweyemamu.

Mwezi Machi mwaka jana Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA), kilifanya utafiti wa kihabari Wilayani Handeni kuangalia matukio ya mimba kwa wanafunzi na kubaini uwepo wa kesi nyingi za wanafunzi kutiwa mimba na kukatishwa masomo.

*Imeandaliwa na www.thehabari.com kwa kushirikiana na TAMWA

Tuesday 2 April 2013

Urafiki wa Walimu na wanafunzi ni muhimu shuleni

Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Msingi King'ongo wakiwa katika picha ya pamoja na mmoja wa walimu wao.

Mbunge Chalinze kuziwekea shule za jimbo lake umeme wa Jua


Mbunge wa Chalinze, Said Bwanamdogo aliyefadhili mradi wa umeme wa jua shuleni.
SHULE zilizopo katika Jimbo la Chalinze Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani zinatarajiwa kunufaika na umeme wa jua.

Umeme huo utaunganishwa na wataalamu kwa ufadhili wa Mbunge wa jimbo hilo, Said Bwanamdogo.

Akizungumza hivi karibuni mjini hapa, Bwanamdogo alisema mkakati huo unatarajia kukamilika muda mfupi ujao baada ya wataalamu hao kukamilisha maandalizi ya awali.

Alisema lengo la kuunganisha umeme huo ni kuongeza ufanisi kwa wanafunzi na walimu katika sekta ya elimu.

Mbunge huyo alisema mbali na shule za jimbo hilo, pia nyumba za walimu zitaunganishwa umeme ili kuwavutia zaidi kufundisha katika shule za jimbo hilo.

“Lengo letu ni kuongeza ufaulu kwa wanafunzi katika jimbo letu, lakini pia kuweka mvuto kwa walimu wanapopangiwa katika shule zetu wasiombe uhamisho, waendelee kufundisha,” alisema.

Pamoja na hayo mbunge huyo aliwasihi wazazi kuwa na ushirikiano wa karibu na walimu wanaopangiwa kufundisha katika shule za maeneo yao, ili waweze kuongeza ufaulu kwa wanafunzi.

Wanafunzi watoro kukiona Tabora



HALMASHAURI ya Wilaya ya Sikonge mkoani Tabora imesema inawasaka watoto 576 ambao hawajaripoti katika shule za sekondari.

Akizungmza na waandishi wa habari jana, Ofisa Elimu wa shule za sekondari Wilaya ya Sikonge Kiyungi Kasswa, alisema watoto hao walifaulu mitihani ya darasa la saba, lakini hadi sasa hawajaripoti shuleni.

Alisema wanafunzi walioripoti shule hadi sasa ni 846 kati ya 1,428 waliofanya mitihani ya kuhitimu darasa la saba mwaka jana.

Kasswa alisema kati watoto 567 ambao hawajaripoti shule, wa kiume ni 287 na wasichana 280.

Alisema wamejiwekea utaratibu ambao utasaidia kuwapata watoto hao na kuwarejesha shule sanjari na wazazi ama walezi wao kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria.

Alisema moja ya mikakati hiyo pia wameagiza viongozi wote kuanzia ngazi ya vitongoji, vijiji na kata kuhakikisha wanaanza kuwasaka watoto wote na wanaripoti shule haraka.

Kasswa aliongeza changamoto moja ambayo mara nyingi imekuwa chanzo cha watoto kukacha shule ni umbali mrefu, kwani watoto wanatembea kilomita zaidi ya 20 hadi 46 kufuata shule.

Hata hivyo, alisema wanajitahidi kuanza ujenzi wa hosteli, hali ambayo itasaidia kupunguza utoro ikiwemo kupikiwa chakula shuleni.





CHANZO:TANZANIA DAIMA

Shule maalum Sikonge yalilia walimu


Picha hii haihusiani na habari hii, ila kwa idadi kubwa ya wanafunzi kama hii walimu watafundishaje?

SHULE ya Msingi Sikonge, iliyopo mkoani Tabora kitengo cha elimu maalumu kwa walemavu, inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwamo ya ukosefu wa walimu.
Afisa Elimu Maalum wilayni Sikonge, Egata Magafu aliwaambia waandishi wa habari mkoani humo kuwa, shule hiyo iliyoanzishwa mwaka 2011 ina walimu watatu, wakati mahitaji halisi kulingana na idadi ya wanafunzi waliopo ni walimu nane.
“Shule kwa sasa ina wanafunzi 52, hivyo wanahitajika walimu nane na watumishi tisa, lakini kwa sasa wako
watatu tu hivyo kuwapa wakati mgumu wanafunzi kupata elimu bora,” alisema.
Mbali na hilo, alisema changamoto nyingine ni upungufu wa vyumba vya madarasa, vitendea kazi na wazazi kuwaficha watoto kutokana na imani potofu.
Alisema wanahitaji vyumba vya madarasa sita, ofisi za walimu mbili, nyumba za watumishi 14 na chumba
kwa ajili ya kufundishia watoto wenye ulemavu wa kutosikia.
Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Elimu Maalumu Wilaya ya Sikonge, Malaki Gumato, alisema
licha ya changamoto hizo, wamefanikiwa kujenga vyumba vya madarasa vinne na bweni moja.
Alisema mafanikio mengine ni kuongezeka kwa wanafunzi kutoka watano shule ilipoanzishwa hadi 52,
kujenga choo chenye matundu manne, kisima kimoja cha maji, tanki la kuvuna maji lenye uwezo wa ujazo
wa lita 5,000 na kufanikiwa kupata baadhi ya vifaa vya kufundishia kwa ajili ya walemavu wa macho.
Shule hiyo ilianzishwa kwa lengo la kutoa elimu kwa walemavu wa macho, albino, wenye uono hafifu na
viziwi.