Sunday 3 November 2013

Wanafunzi zaidiya 100 wafungiwa chumba kimoja kwa saa tano

Picha haihusiani na habari hii
WANAFUNZI zaidi ya 100 wa Shule ya Msingi ya kutwa ya St. John Bosco, Kibaha mkoa wa Pwani, wanadaiwa kufungiwa kwenye chumba kimoja cha shule hiyo kwa muda wa saa tano kama adhabu ya kutolipa ada.
Tukio hilo limetokea juzi ambapo wanafunzi hao wanadai kufungiwa katika chumba hicho na Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo, kuanzia saa 2:00 asubuhi hadi saa 7:00 mchana.
Wanafunzi hao wanadaiwa ada kati ya Sh. 50,000 hadi Sh. 400,000. Ada ya mwaka katika shule hiyo kwa mwanafunzi mmoja ni Sh. 1,300,000.
Wazazi wa wanafunzi hao wakizungumza na NIPASHE jana mjini Kibaha, walisema walipewa taarifa na watoto wao kwamba walifungiwa ndani ya chumba kwa sababu hawajalipa ada ya shule, jambo ambalo limewasikitisha sana na kinyume na haki za binadamu.
“Ukatili waliofanyiwa watoto wetu katika shule hii haujatufurahisha kabisa, kwani shule hii ni ya kidini sasa inakuaje Mwalimu Mkuu anakosa roho ya subira,” walisema wazazi hao ambao walikuwa wamejikusanya kutafakari kwa kina jambo hilo.
Walisema baada ya kupata taarifa kwa barua kutoka kwa uongozi wa shule kwamba wanatakiwa kuwalipia ada watoto wao, waliomba wawasilishe ada hiyo wiki ijayo lakini wameshangazwa na kitendo cha uongozi cha kukosa subira na kuamua kuwafanyia kitendo cha ukatili watoto wao.
“Ada yenyewe tunayodaiwa tulipe imetokana na ongezeko la ada kutoka Sh. 850,000 tuliyokuwa tukilipa awali na kufikia Sh. 1,300,000 kwa mwaka ambayo imepandishwa ghafla, kwanza watoto wenyewe wanapewa chai ya rangi na mikate tu saa 4:00 asubuhi,” walisema wazazi hao waliokuwa na jazba.
Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo, Sista Fabiola alipoulizwa kuhusu madai hayo alisema si ya kweli kwa sababu shule haina chumba cha kuweza kuwafungia wanafunzi hao kama inavyodaiwa na wazazi.
Alisema wapo watoto ambao wanadaiwa ada toka Januari hawajalipa na wazazi wao wamekuwa wakipewa barua mara kwa mara kila shule inapofungwa na kufunguliwa, lakini baadhi yao wamekuwa wakorofi.

CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

Dk Slaa aponda mfumo mpya wa ufaulu

Dk Slaa
SIKU tatu baada ya serikali kutangaza mfumo mpya wa madaraja ya ufaulu, licha ya kupingwa na wengi, kitendo hicho pia kimemhuzunisha Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa.

Akizungumza na gazeti hili jana, Dk. Slaa alisema:  “Kwa kubadili mfumo wa maksi serikali sasa bila huruma imeamua kwa makusudi kabisa kuua ubora wa elimu nchini, ni kweli kwa kupanua wigo wa kufaulu serikali haitalaumiwa kwa akili ya kawaida, itaonekana  wamefaulu wote, lakini elimu haitawasaidia watoto wenyewe, haitawasaidia wazazi wenyewe,  na haitasaidia taifa letu. Tutapataje madaktari bora, tutapataje wanasayansi, walimu au wahandisi bora?  Mabadiliko yanahitajika kusaidia taifa hili lisizikwe na watu wasio na huruma.”

Kwa upande wake, Dk. George Kahangwa, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam akizungumza kupitia kipindi cha ‘Tuongee’ kinachorushwa na Star TV,  alisema  hatua ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Profesa Sifuni Mchome, kutangaza mageuzi hayo ni kuonesha ni jinsi gani serikali  imeshindwa kutatua mzizi  wa tatizo la elimu nchini na baadala yake inatapatapa kwa kuja na sera iliyoiacha kuitumia toka mwaka 1995 iliyotumia alama hiyo ya 50 kwa 50  kwa Tanzania Bara na 40 kwa 60, kwa Visiwani Zanzibar ambapo safari hii imeamua kuitumia tena na kuiweka wazi.

Dk. Kahangwa alisema serikali licha ya kutoa tamko la kubadilisha daraja jipya huku ikikiri kuwa ilikuwa ikitoa alama za kuanzia 75 hadi 100 ndio ufaulu wa alama ‘A’ na daraja la kwanza, pasipo kuiweka wazi kwa muda mrefu, sasa wameamua kuiweka wazi, huku ni kuwaada Watanzania kwa kutumia sera ambayo hazitekelezeki.

“Hili ni janga la elimu, huko nyuma waliondoa ‘sifuri’ kwenye ufaulu na kuweka ‘feli’, leo hii wanakuja tena na kuongezea daraja la tano na kuita ‘ufaulu hafifu au ufaulu usioridhisha’, huku ni kucheza na masuala ya msingi katika taifa. Kuja mbele za umma na kutangaza tena juu ya sera hiyo waliyoiacha kwa muda pasipokuitumia ni jinsi gani sera hiyo haitekelezeki tena,” alisema Dk. Kahangwa.

Dk. Kahangwa amewaomba Watanzania na wadau wa habari nchini kujitokeza kuwahoji wadau wa elimu kama walishirikishwa kwenye kupitishwa kwa mabadiliko hayo.

Dk. Kahangwa alisema  hivi karibuni kuna shirika lilifanya utafiti wa shule za sekondari 100 ambapo shule nne tu ndizo zinahesabika kama shule bora huku 96 zikihesabika kama makambi ya shule.

Hata hivyo, Mhariri Mtendaji wa gazeti la Tanzania Daima, Ansbert Ngurumo, aliyekuwapo kwenye mahojiano hayo alifananisha kitendo cha serikali kupanga madaraja hayo kuwa ni sawa na kupanua magoli ya uwanja ili kila mchezaji afunge, huku akiitaka serikali iwaombe radhi wananchi kwa kuwa ilianza kutumia mfumo huo bila kuwaarifu.

Naye Mratibu wa Chama cha Waandishi wa Habari mkoani Mwanza, Edwin Soko, alisema mabadiliko haya yaliyolenga kuongeza idadi ya wahitimu bila kuangalia uzoefu, yamesababisha taifa kukosa falsafa na Dira ya Taifa.

Harambee ya Chuo cha Mwika yakwama, kisa...!

CHUO cha Uhifadhi na Usaimamizi wa Wanyamapori, Mweka cha mkoani Kilimanjaro kimesherehekea miaka 50 tangu kuanzishwa kwake kwa kukwama kuendesha harambee kama ilivyopangwa.

Harambee hiyo ilikuwa ifanyike chuoni hapo juzi baada ya kumalizika kwa mkutano wa wataalamu wa usimamizi na uhifadhi wa wanyamapori kutoka nchi za Scandinavia, Bara la Ulaya, Amerika na Afrika, ilikuwa na lengo la kuchangisha kiasi cha dola milioni 3.6 za Marekani kwa ajili ya upanuzi wa chuo hicho.

Kwa mujibu wa ratiba ya shughuli hiyo ya harambee, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alitarajiwa kuwa mgeni rasmi huku uongozi wa chuo hicho ukiwaalika wageni wengine mashuhuri akiwemo waziri mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa na Mwenyekiti wa kampuni za IPP, Reginald Mengi.

Katika hali isiyo ya kawaida hadi muda wa kuanza kwa shughuli hiyo saa saba mchana hakukuwa na mgeni hata mmoja kati ya walioalikwa aliyewasili chuoni hapo na badala yake walionekana walimu na wanachuo tu.

Wakati hali ikiwa hivyo, katika uwanja wa michezo wa chuo hicho ambako kulipambwa kwa ajili ya tukio hilo licha ya kutokuwepo kwa wageni waalikwa Tanzania Daima Jumapili lilishuhudia viti vikiwa wazi licha ya uwepo wa vifaa vya muziki vilivyokuwa vikipiga muziki na matangazo yakiita watu uwanjani hapo.

Hata hivyo ilipotimu saa 8 mchana aliwasili Mbunge wa Kahama, James Lembeli na Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe aliyedaiwa kumwakilisha Pinda.

Baada ya kuwasili Maghembe alipokewa na wafanyakazi wa chuo hicho akiwamo Kaimu Mkuu wa Chuo, Dk. Freddy Manonge, aliyeambatana naye hadi ofisi kuu ya chuo kwa ajili ya kupatiwa maelezo mafupi.

Mazungumzo kati ya Waziri Maghembe na uongozi wa chuo yalichukua muda mrefu, hali iliyolazimu gazeti hili kutaka kujua nini kinaendelea na baada ya kufika katika ofisi hiyo mmoja wa wafanyakazi wa chuo hicho alijibu kwa kifupi: ‘Kuna kikao tutawaita’.

Baada ya kusubiri hadi saa 11 jioni, Lembeli ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge inayoshughulikia Maliasili na Utalii alitoka ndani ya ofisi hiyo kisha akatoka makamu mkuu wa chuo akiambatana na Ofisa Uhusiano wa chuo hicho, Richard Kisasembe.

Mkuu wa chuo hicho baada ya kufanya mawasiliano na mshereheshaji wa shughuli aliyefahamika kwa jina moja la Peter baadaye alitoa tangazo la mabadiliko akisema kutokana na watu wengi waliokuwa wamealikwa kupata dharura hivyo shughuli ya harambee imehairishwa.

“Baada ya watu wengi kupata dharura wale ambao tumekuja leo kwa ajili ya kuchangia basi tunaomba waende ofisini ili kwenda kutoa ahadi zenu pale na kesho (jana) tutatangaza kiasi kilichopatika kwa hiyo suala la harambee tutalikamilisha kesho,” alisema mshereheshaji Peter.

Akizungumzia hali hiyo, Profesa Maghembe alisema alimwakilisha Waziri Mkuu Pinda ambaye ametingwa na shughuli za Bunge.

Kuhusu ujangili, Profesa Maghembe alisema lipo tatizo katika nchi za Afrika, wapo watu wenye uchu wa kujipatia mali kwa haraka, ambao wanataka kumaliza rasilimali za wanyamapori waliotunzwa kwa ghamara na muda mrefu.
TANZANIA DAIMA

Wanawake wajasiriamali waasa juu ya bidhaa zao

DSC_0394
Mama Tunu Pinda akikaribishwa kufunga maonyesho ya wiki ya Wakinamama Wajasiriamali na Mratibu wa Kitaifa wa Programu ya kuendeleza wajasirimali wanawake Tanzania kutoka ILO, Noreen Toroka. kushoto kwa Mama Pinda ni Mwenyekiti wa MOWE, Bi Elihaika Mrema na
DSC_0354
Mke wa Waziri Mkuu, Mama Tunu Pinda akifunga rasmi Maonyesho ya Wanawake Wajasirimali (MOWE) katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam, maonyesho hayo ya wanawake wajasiriamali yalikuwa ya wiki nzima ambapo wakinamama wanapata nafasi ya kuonyesha na kuuza bidhaa mbalimbali Usindikaji, Mvinyo, Batiki kwa wakazi wa jijini.
DSC_0337
Mratibu wa Kitaifa wa Programu ya kuendeleza Ujasiriamali kwa wanawake Tanzania toka Shirika la Kazi Duniani (ILO) Noreen Toroka akizungumza wakati hafla ya kufunga maonyesho hayo ambapo amesema wiki nzima ilikuwa ni maonyesho wanawake toka sehemu mbalimbali nchini Bara na Visiwani wamepata wasaa wakubadilishana mawazo na mbinu za Kibiashara.
DSC_0324
Mwenyekiti wa Kamati ya MOWE, Mama Elihaika Mrema akizungumza wakati wa kufunga maonyesho hayo ya Wajasirimali wakinamama jijini Dar es Salaam.
DSC_0287
Mama Tunu Pinda akitembelea baadhi ya mabanda katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar.
DSC_0302
Mama Tunu Pinda akipata maelezo kwa mmoja wa Wajasirimali Wanawake walioshiriki maonyeshio hayo.

SOMA MATOKEO YA DARASA LA 7 YA MWANAO HAPA


Dar es salaam, Tanzania
MATOKEO ya Darasa la Saba yametangazwa  na mwaka huu huku ufaulu ukiwa umeongezeka kutoka asilimia 30.72 mwaka jana mpaka asilimia 50.61 mwaka huu kutokana na wanafunzi walio fanya mtihani mwaka huu wa darasa la saba wamefaulu zaidi ukilinganisha na wanafunzi wa mwaka jana Kaimu mtendaji wa Baraza la Mtihani Charles Msonda amesema ufaulu katika masomo yote umepanda kwa asilimia kati ya 6.01 na 28.06 ukilinganisha na mwaka 2012.
Mwaka huu watahiniwa wamefahulu zaidi katika somo la Kiswahili kwa asilimia 69.06 na somo walilio faulu kwa kiwango kidogo zaidi ni somo la Hisabati wamefaulu kwa asilimia 28.62.
 Msonda amesema jumla ya watahiniwa 427,606 kati ya 844,938 walio fanya mtihani huo wamepata alama ya 100 kati ya alama ya 250 idadi hiyo ni sawa na asilimia 50.61

Matokeo darasa la 7 yatia fora


Baadhi ya wanafunzi hao walipokuwa wakifanya mtihani huo hivi karibuni.
Wakati wanafunzi wa Kidato cha Nne wakianza mitihani yao kesho, Baraza la Mitihani la Tanzania  (NECTA) limetangaza matokeo ya darasa la saba mwaka huu.
Matokeo hayo yanaonesha ufaulu umeongezeka kwa asilimia 19. 89, tofauti na ilivyokuwa mwaka jana.
Katika matokeo hayo, wanafunzi 13 wamefutiwa matokeo, kutokana na udanganyifu ambapo watano walikariri mtihani kwa kufanya mara tatu mwaka 2011, 2012 na mwaka huu. Wengine nane walikutwa na vikaratasi vya majibu katika chumba cha mitihani.
Kaimu Katibu Mtendaji wa Baraza hilo, DK Charles Msonde alitangaza matokeo hayo jana.
Alisema jumla ya watahiniwa 427,606, kati ya 844,938 waliofanya mtihani, wamepata alama zaidi ya 100 katika alama 250, idadi ambayo ni sawa na asilimia 50.61.
Alisema kati yao, wasichana ni 208,227 ambao ni sawa na asilimia 46.68 na wavulana ni 219,379 sawa na asilimia 55.01 huku miongoni mwao wamo wenye ulemavu 476, wasichana wakiwa 219 na wavulana 257.
“Mwaka jana asilimia ya watahiniwa waliopata alama zaidi ya 100 ilikuwa 30.72, hivyo kuna ongezeko la asilimia 19.89 huku takwimu za masomo zikionesha ufaulu katika masomo yote, umepanda kwa asilimia 6.01 na 28.06, ikilinganishwa na mwaka jana,”alisema.
Alibainisha kuwa watahiniwa wamefaulu zaidi katika somo la Kiswahili, ambapo ufaulu ni asilimia 69.06.  Somo walilofaulu kwa kiwango cha chini ni Hisabati, lenye ufaulu wa asilimia 28.62.
Msonde alisema matokeo ya mwaka huu yamewahi, kutokana na watahiniwa kufanya mitihani kwa mara ya pili kwa kutumia Karatasi Maalum za Optical Mark Reader (OMR), ambazo zilisahihishwa kwa kutumia mfumo wa kompyuta.
Alisema washiriki 301 walishiriki katika usahihishaji, ikilinganishwa na washiriki zaidi ya 4,000 waliokuwa wakishiriki kabla ya kuanza kwa mfumo huo. Kwa mwaka huu, usahihishaji umefanywa kwa siku 16, ukilinganishwa na siku 30 zilizotumika awali.
Dk Msonde alisema ili kuhakiki usahihishaji kwa kutumia mfumo wa kompyuta, sampuli ya karatasi 20,795 za majibu kutoka shule 200 katika wilaya 48 za mikoa tisa, zilisahihishwa kwa mkono na kufanyiwa ulinganifu na kusahihishwa kwa kompyuta.
Alisema usahihishaji wa kompyuta, ulikuwa sahihi huku usahihi wa kutumia kalamu ukiwa na makosa ya kibinadamu katika karatasi 249, sawa na asilimia 1.2.
DK Msonde alisema jumla ya watahiniwa 867,983 wa shule za msingi, walisajiliwa kufanya mtihani huo, wakiwemo wasichana 455,896 sawa na asilimia 52.52 na wavulana 412,089 sawa na asilimia 47.48. Kati ya hao, watahiniwa 597 walikuwa wenye uono hafifu na watahiniwa 88 walikuwa wasioona.
Alisema watahiniwa 844,000, sawa na asilimia 97.34 ya waliosajiliwa, walifanya mitihani, kati yao wasichana walikuwa 446,115 sawa na asilimia 97.85 na wavulana 398,823 sawa na asilimia 96.78 .
Alisema watahiniwa 23,045 sawa na asilimia 2.66, hawakufanya mtihani, kutokana na sababu mbalimbali, zikiwemo utoro na ugonjwa. Kati yao, 9,781 sawa na asilimia 2.15 ni wasichana na 13,264  sawa na asilimia 3.22 ni wavulana.
Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Shule na Vyuo Binafsi Tanzania (TAMONGSCO), Mahmoud Mringo alisema shule binafsi zimeongoza katika matokeo hayo kwa kila somo.
Alisema katika somo la Kiswahili, shule binafsi wamepata asilimia 98 wakati za Serikali asilimia  68, na kwa Kingereza shule binafsi asilimia 99 na Serikali 33.
Kwa somo la Maarifa ya Jamii, shule binafsi asilimia 86 Serikali 52 , Hisabati shule binafsi asilimia 81 na Serikali 27 na somo la Sayansi, shule binafsi asilimia 84 na Serikali 46.

Serikali yatangaza viwango vipya vya ufaulu mitihani ya taifa

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA 
WIZARA YA ELIMU NA MAFUNZO YA UFUNDI
Wizara imekusanya maoni ya Wadau wa Elimu kuhusu Upangaji wa Viwango vya Alama (Grade Ranges) katika Mitihani ya Kuhitimu Kidato cha Nne na cha Sita pamoja na Matumizi ya Alama za Tathmini Endelevu ya Mwanafunzi (Continuous Assessment ama CA) kwa ajili ya kuamua kiwango cha ufaulu wa mwanafunzi. Maoni ya wadau yamekusanywa kwa sababu kwa muda mrefu sasa upangaji wa viwango vya alama vinavyotumika na utaratibu wake katika mitihani ya kuhitimu Kidato cha Nne na Kidato cha Sita umekuwa haufanani pamoja na kwamba mitihani hiyo yote ni ya elimu ya sekondari. Pia mfumo masuala mbalimbali ya mitihani katika elimu ya sekondari umekuwa na miundo tofauti ikiwemo ule unaotumika shuleni na ule wa Baraza la Mitihani la Taifa. Kwa sasa kuna miundo mikuu miwili katika mfumo huo.
 
Muundo wa Kwanza ni upangaji wa viwango katika ngazi ya Shule ambapo Alama Mgando (Fixed Grade Ranges) zifuatazo hutumika kupanga madaraja: A = 81 – 100; B = 61 – 80; C = 41 – 60; D = 21 – 40 na F = 0 – 20. Muundo huu umetumika kwa muda mrefu na umezoeleka kwa walimu na wanafunzi wa elimu ya sekondari kwa ujumla.
Muundo wa Pili ni wa viwango vinavyotumiwa na Baraza la Mitihani la Taifa ambapo ambapo kabla ya mwaka 2012 muundo wa viwango nyumbufu (flexible grade ranges) ulitumika. Katika muundo huu uwigo wa alama ulibadilika badilika kulingana na hali ya matokeo ilivyokuwa kwa mwaka husika. Lakini kuanzia mwaka 2012, Serikali iliamua kutumia mfumo wa Upangaji wa Alama Mgando (Fixed Grade Range) kwa Kidato cha Nne na Kidato cha Sita. Katika mtihani wa Kidato cha Nne mwaka 2012 Baraza lilitumia mfumo huu wa alama mgando ambapo: A = 80 – 100, B = 65 – 79, C = 50 – 64, D = 35 – 49, F = 0 – 34. Kwa upande wa Kidato cha Sita Baraza lilitumia mfumo wa A = 80 – 100; B = 75 - 79; C = 65 – 74; D = 55 – 64; E = 45 – 54; S = 40 – 44 na F = 0 – 39. Mifumo hii ya Baraza haikuwa inafahamika kwa wadau na hivyo kuwa sehemu ya malalamiko katika sekta ya elimu na mafunzo.
Vilevile, Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 1995 imeelekeza kwamba katika kuamua kiwango cha ufaulu wa mwanafunzi wa elimu ya sekondari, Alama za CA zitachangia asilimia hamsini (50%) na Mtihani wa mwisho utachangia asilimia hamsini (50%). Kwa upande wa Zanzibar, CA zimekuwa zikiandaliwa kwa mfumo wa asilimia arobaini (40%) na mtihani wa mwisho asilimia sitini (60%). Pamoja na kwamba Baraza halijawahi kuutumia mifumo hii tangu ilipowekwa, kumekuwa na mitazamo, maoni na mapendekezo tofauti katika muundo na matumizi ya alama za CA. Kuna mawazo pia kwamba mfumo wa CA kuchangia matokeo ya mwisho ya mwanafunzi pia utumike kwa watahiniwa wa kujitegemea (private candidates).
 Kwa sasa matokeo ya mitihani ya watahiniwa hawa yamekuwa yakitumia alama za mtihani wa mwisho tu na hivyo kutafsiriwa kama utaratibu ambao unamwonea mwanafunzi ambaye anahamu ya kujiendeleza kielimu lakini anakwama kwa sababu mfumo unaotumika siyo rafiki kwa mtahiniwa.
Kwa mantiki hii, Wizara imedhamiria kufanya harmonization ya masuala ya alama katika mitihani ya Kidato cha Nne na Kidato cha Sita ili kupata muundo mmoja na ulio wazi kwa wadau wote wa elimu ya sekondari. Lakini pia serikali imedhamiria kuhakikisha tathmini za wanafunzi katika ngazi mbalimbali zinakwenda sambamba na matarajio ya mitaala inayotumika na ambayo inahuishwa mara kwa mara ili iendane na wakati na mahitaji ya elimu katika ngazi mbalimbali.
VIWANGO NA UTARATIBU KUANZIA MWAKA 2013 KWA KIDATO CHA NNE NA MWAKA 2014 KIDATO CHA SITA
Baada ya kufanya tathmini ya maoni mbalimbali ya wadau, misingi ifuatayo ilizingatiwa katika maamuzi kuhusu makundi ya alama na muachano wake:
a)      Alama zitakazotumika zitakuwa A, B, C, D, E na F. Muachano wa alama kati ya kundi moja hadi jingine utafanana, isipokuwa tu pale ambapo itaonekana kuna sababu na hakuna athari za kuwa na muachano tofauti na ule ambao umetumika katika makundi mengine.
b)      Makundi ya alama hayatakuwa na clusters isipokuwa pale ambapo itaonekana kufanya hivyo kunaleta tija katika kupata picha ya wahitimu kwa ajili ya matumizi mbalimbali. Kwa mantiki hii
(i)         makundi ya alama A, C, D, E na F yabaki na cluster moja moja bali kundi la alama Blitakuwa na clusters mbili. Kundi la kwanza litakuwa la wale ambao wamepata alama kati ya 50 mpaka 59 na litaitwa B na lingine litakuwa la wale ambao wamevuka uwigo wa 50 hadi 59 na kuelekea uwigo wa 60 hadi 74 na hili litaitwa B+ (angalia jedwali hapo chini).

(ii)        Pamoja na kuwa na muachano wa alama 26 kama jedwali linavyoonesha hapo chini, alama A kwa miaka mingi imekuwa ikianzia alama 75 hadi 100 na kwamba pamoja na uwigo huo bado wanaofaulu kwa kiwango hicho ni wachache sana. Kwa mantiki hii, hakuna haja ya kubadilisha uwigo ila juhudi ziendelee katika ufundishaji na ujifunzaji ili kiwango cha ufaulu kiongezeke na kupata wanafunzi wengi zaidi wanaofaulu katika kundi hili.

(iii)       Pia, pamoja na kuwa na muachano wa alama 20 kama jedwali linavyoonesha hapo chini kwa miaka mingi, huko shuleni mwanafunzi aliyepata alama 21 na hadi 30 alihesabiwa kuwa na ufaulu wa chini kabisa au hafifu kwa kiwango cha alama na ingawa ilikubalika ufaulu wa aina hiyo kwa mazingira ya nchi yetu unaridhisha. Alama F ilikuwa ni kwa wale waliopata chini ya hapo. Hivyo, alama F itaendelea kuwepo na itaanzia alama 0 hadi 19 na E itaanzia alama 20 hadi 29 na D – 30 -39. Lengo la muundo huu ni kuwa alama mbalimbali, isipokuwa kwa makundi machache, zianzie kwenye 0 yaani 0, 10, 20, 30, 40 na kuendelea badala ya kuanzia kwenye moja yaani 1, 11, 21, 31, 41 na kuendelea. Hii ni kwa ajili ya kuleta mtizamo unaofanana katika ngazi mbalimbali za elimu ambapo kwa sasa ngazi ambazo siyo za elimu msingi na sekondari zinatumia muundo wa kuanzia kwenye 0 badala ya 1. 
c)      Uwigo wa jumla wa alama kwa Kidato cha Nne na Kidato cha Sita utaendelea kuwa wa alama 0 hadi 100 na kila kundi katika uwigo huu limepewa tafsiri kwa ajili ya kuamua mambo mbalimbali yanayohusu maendeleo ya mwanafunzi kulingana na malengo ya mtihani husika. Kimsingi, tafsiri zifuatazo zitakatumika
(i)         Alama A itakuwa na maana ya ufaulu uliojipambanua (distincion or outstanding performance),
(ii)        Alama B+ itakuwa na maana ya ufaulu bora sana (excellent performance),
(iii)       Alama B itakuwa na maana ya ufaulu mzuri sana ( very good perfomance),
(iv)       Alama C itakuwa na maana ya ufaulu mzuri (good performance);
(v)        Alama D itakuwa na maana ya ufaulu wa wastani (low performance),
(vi)       Alama E itakuwa na maana ya ufaulu hafifu (very low performance), na
(vii)      Alama F itakuwa na maana ya ufaulu usioridhisha (unsatisfactory performance). 
Wataalamu katika maeneo mbalimbali ya elimu na ulimwengu wa kazi, kwa kushirikiana na Wizara, watatoa maana ya tafsiri hizi kiutendaji katika maeneo yao kulingana pia na mahitaji yao.
d)      Alama C iwe ndiyo alama ya ufaulu mzuri ambao hauhitaji urekebu wa lazima, wakati alama D na E ni alama za ufaulu unaohitaji urekebu kadri mwanafunzi atakavyokuwa anaendelea na masomo ili kuthibitisha kama mlengwa anaweza na kulingana na mahitaji ya eneo husika (targeted remediation). Alama F iwe alama ya eneo linalohitaji urekebu wa hali ya juu (intesive remediation) ili mwanafunzi huyo aweze kumudu masomo kadri anavyoendelea kukua kielimu ama atakapoingia katika ulimwengu wa kazi.
e)      Makundi ya alama yatajumuisha CA kwa kiwango cha asilimia isiyozidi 40 na mtihani wa mwisho kwa asilimia isiyozidi 60 kwa makundi yote ya watahiniwa ikiwemo wale wa kujitegemea (private candidates). Hii ni kwa kuzingatia kwamba CA siyo vizuri izidi uwigo wa alama ya ufaulu mzuri unapoanzia ambayo ni C au 40.
f)       CA kwa upande wa Kidato cha Nne zitokane na mtihani wa Kidato cha Pili (alama 15), matokeo ya Kidato  cha Tatu (alama 5 kwa kila muhula, na hivyo jumla ya alama 10), mtihani wa Mock (alama 10) na kazi mradi  auProjects (alama 5). Kwa upande wa Kidato cha Sita, CA iendelee kutokana na muundo unaotumika sasa.
g)      CA zitumike pia kwa watahiniwa wa kujitegemea. Kwa upande wa watahiniwa wa kujitegmea ambao wanarudia Mitihani, CA zao  zitumike zile zilizotumika kutoa matokeo yake ya mitihani ya awali.  Kwa watahiniwa wa kujitegemea waliopitia mfumo wa Qualifying Test (QT), matokeo ya QT yatumike kama CA na mtihani wa mwisho uchangie alama 60.
h)      Kwa vile alama endelevu kwa mwaka 2013 kwa wanafunzi wa Kidato cha Nne tayari zimeshawasilishwa Baraza la Mitihani  Tanzania, alama hizo zichangie asilimia 40 katika mtihani wa Kidato cha Nne mwaka 2013.
i)        Muundo wa wastani wa alama katika ufaulu (Grade Points Average ama GPA) utaandaliwa na kuanza kutumika pale utakapokuwa tayari na wadau wataelimishwa kuhusu muundo huo ili wapate kuufahamu na manufaa yake katika elimu ya sekondari.
j)        Muundo huu mpya wa alama utatumika kwa mzunguko wa miaka minne kabla haujahuishwa tena ili kuupa muda wa kutosha kuona aina ya changamoto zinazojitokeza na jinsi ya kuzishughulikia. Aina hii ya muda itaruhusu vidato vinne vya elimu ya sekondari ya kawaida na nane ya elimu ya sekondari ya juu kupimwa. Hata hivyo, uhusihaji wa masuala ya mitihani unaweza ukafanyika iwapo matokeo ya uhuishaji wa mitaala kwa ujumla utahitaji pia eneo la mitihani liguswe na kuhuishwa pia.
Kwa mantiki hii, viwango vya alama na ufaulu ni kama inavyooneshwa kwenye jedwali la 1 hapa chini:
Jedwali Na 1
MUUNDO WA ALAMA NA UFAULU
ALAMA
UWIGO WA ALAMA
IDADI YA ALAMA
TAFSIRI
A
75 - 100
26
Ufauli Uliojipambanua
B+
60 - 74
15
Ufaulu bora sana
B
50- 59
10
Ufaulu mzuri sana
C
40 - 49
10
Ufaulu mzuri
D
30 - 39
10
Ufaulu Hafifu
E
20 - 29
10
Ufaulu hafifu sana
F
0 - 19
20
Ufaulu usioridhisha
Kwa aina hii ya muundo wa alama, na kwa kuwa muundo wa GPA utaanza kuandaliwa na wadau kuelimishwa kabla haujaanza kutumika, katika kipindi hiki mpaka wakati huo, muundo wa madaraja utakuwa kama inavyooneshwa kwenye jedwali la 2 hapa chini.
Jedwali Na 2
MUUNDO WA MADARAJA
MUUNDO WA ZAMANI
MUUNDO MPYA
MAELEZO
POINTI
DARAJA
POINTI
DARAJA
7-17
1
7-17
I
Kundi la ufaulu uliojipambanua na bora sana
18-21
II
18-24
II
Kundi la ufaulu mzuri sana
22-25
III
25-31
III
Kundi la ufaulu mzuri na wa wastani
26-33
IV
32-47
IV
Kundi ufaulu hafifu
34-35
0
48-49
V
Kundi la ufaulu usioridhisha

Wataalamu wa mifumo ya mitihani watalifanyia kazi zaidi jedwali hili la madaraja ili liweze kutumika kwa ufanisi katika kipindi hiki cha mpito.
Kwa mantiki hii, Daraja Sifuri linafutwa na kuwekwa daraja litakalojulikana kama Daraja la Tano na ambalo litakuwa ndilo la mwisho kabisa katika ufaulu.
HITIMISHO
Mabadiliko haya yamefanyika ili kuendelea kuimarisha mfumo wetu wa elimu na kuweka wazi taratibu mbalimbali kwa ajili ya mitihani na masuala mengine. Yako mambo mengi mengine ambayo hayana budi kuendelea kuimarishwa ikiwemo mfumo wa mitaala, walimu, mazingira ya kujifunzia na kufundishia pamoja na vitabu na vifaa vingine muhimu katika elimu. Masuala haya yanaendelea kuangaliwa kupitia mikakati mbalimbali ikiwemo mpango wa Matokeo Makubwa Sasa ama Big Results Now (BRN). Ushirikiano wa wadau wote ili kuleta tija kwenye elimu ni muhimu sana na hivyo wizara itaendelea kuwashirikisha wadau wote kwa kadri itakavyohitajika na wadau pia wanaombwa wasiache kuishirikisha wizara pale watakapokuwa na jambo lolote ambalo linahitaji ushirikiano ili kwa pamoja tuweze kupata mafanikio katika sekta ya elimu.
Imetolewa,
KATIBU MKUU
WIZARA YA ELIMU NA MAFUNZO YA UFUNDI